Ijumaa, Novemba 14
Kujipamba kwenu kusiwe kwa nje.—1 Pet. 3:3.
Usawaziko unatusaidia kuheshimu maoni ya wengine. Kwa mfano, kuna akina dada ambao wanapenda kujipamba usoni, na kuna wengine ambao hawapendi. Baadhi ya Wakristo hufurahia kunywa kileo kwa kiasi, lakini wengine huamua kwamba hawatakunywa. Wakristo wote wanatamani kuwa na afya nzuri, lakini wanachagua aina mbalimbali ya matibabu. Ikiwa tunafikiri kwamba sikuzote sisi tuko sahihi, huenda tukajaribu kuwashawishi wengine wafuate maoni yetu, jambo ambalo linaweza kuwakwaza wengine na kusababisha migawanyiko. (1 Kor. 8:9; 10:23, 24) Kwa mfano, badala ya kutupatia sheria kali kuhusu jinsi tunavyopaswa kuvaa, Yehova anatupatia kanuni. Tunapaswa kuvaa kwa njia ambayo inamfaa mtumishi wa Mungu, inayoonyesha usawaziko, kiasi, na “utimamu wa akili.” (1 Tim. 2:9, 10) Kwa hiyo, hatujielekezei fikira wenyewe kupitia jinsi tunavyovaa. Kanuni za Biblia pia zitawasaidia wazee wa kutaniko waepuke kuweka sheria zao wenyewe kuhusu mavazi na mitindo ya nywele. w23.07 32:13-14
Jumamosi, Novemba 15
Nisikilizeni kwa makini, mle kilicho chema, nanyi mtafurahia sana vitu vyenye lishe kwelikweli.—Isa. 55:2.
Yehova anatuonyesha jinsi tunavyoweza kuwa na wakati ujao wenye furaha. Wale wanaokubali mwaliko unaotolewa kwa sauti kubwa na “mwanamke mpumbavu,” wanakazia fikira kujifurahisha kupitia ukosefu wa maadili kisiri. Matendo yao yatawaongoza katika “vina vya Kaburi.” (Met. 9:13, 17, 18) Matokeo ni tofauti kabisa kwa wale wanaokubali mwaliko wa “hekima ya kweli”! (Met. 9:1) Tunajifunza kupenda mambo ambayo Yehova anapenda na kuchukia mambo ambayo anachukia. (Zab. 97:10) Na tunafurahi kuwaalika wengine ili waje na kunufaika kutokana na “hekima ya kweli.” Ni kana kwamba tunaita “kwa sauti [hivi] kutoka vileleni juu ya jiji: ‘Yeyote ambaye ni mjinga na aje humu.’” Sisi na wale wanaokubali mwaliko huo hatunufaiki tu sasa. Tutaendelea kunufaika na kuishi milele ‘tunapotembea moja kwa moja katika njia ya uelewaji.’—Met. 9:3, 4, 6. w23.06 28:17-18
Jumapili, Novemba 16
Mtu asiyekasirika upesi ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu, na mtu anayedhibiti hasira yake ni bora kuliko mtu anayelishinda jiji.—Met. 16:32.
Unahisije mfanyakazi mwenzako au mwanafunzi mwenzako anapokuuliza kuhusu imani yako? Je, unapatwa na wasiwasi? Wengi wetu huhisi hivyo. Lakini swali hilo linaweza kutusaidia kutambua mambo ambayo mtu huyo anafikiri au kuamini na kutupatia nafasi ya kuhubiri habari njema. Hata hivyo, nyakati nyingine mtu anaweza kuuliza swali kwa njia inayoweza kutokeza mabishano. Hilo halipaswi kutushangaza. Kwa sababu, baadhi ya watu wameambiwa habari za uwongo kuhusu mambo tunayoamini. (Mdo. 28:22) Isitoshe, tunaishi katika “siku za mwisho,” kipindi ambacho wengi ‘hawataki makubaliano yoyote’ na hata ni “wakali.” (2 Tim. 3:1, 3) Huenda ukajiuliza hivi, ‘Ninawezaje kujibu kwa neema na kwa njia isiyo ya ukali mtu anapopinga imani yangu inayotegemea Biblia?’ Ni nini kitakachokusaidia? Upole utakusaidia. Mtu mwenye sifa ya upole hakasiriki upesi na ana uwezo wa kujizuia anapochokozwa au ikiwa hajui jinsi ya kujibu. w23.09 39:1-2